Mkuu  wa Kurugenzi ya Mifumo ya Uchaguzi Tume ya Uchaguzi Zanzibar Bi. Mwanakombo  Machano Abuu amewataka wafanyakazi waliochaguliwa  kuandikisha Wapiga Kura Wapya katika Daftari la Kudumu linalotarajiwa kuanza tarehe 2 Disemba 2023 kuhakikisha kila mwenye sifa ya kuandikishwa anaandikishwa na kuachana na ushabiki wa Kisiasa kwani zoezi hilo  halihitaji ushabiki wa kisiasa.

Hayo  aliyasema huko kwenye Ukumbi wa kiwanda cha Mafuta ya Makonyo Wawi alipokuwa  akizungumza na Wakuu wa vituo vya Uandikishaji na Makarani wa Uandikishaji  waliochaguliwa kwa zoezi hilo.

Alisema Uandikishaji utaanzia katika Wilaya ya Micheweni hivyo aliwataka kila mmoja kuelekeza akili yake katika kazi hio muhimu ya taifa kwa kuzingatia uadilifu na kumpa kila mwenye haki yake ya kuandikishwa aandikishwe ili awe miongoni mwa Wazanzibar watakaokuwa Wapiga Kura kwa kuwemo ndani ya daftari hilo la Kudumu la Wapiga Kura.

Alisema “Niwaombe sana jiepusheni na kushabikia vyama wakati wa Uandikishaji kwani kufanya hivyo kunaweza kulitia dosari zoezi zima la Uandikishaji”

Alisema kuhakikisha wanafanya kazi vizuri kwenye zoezi la Uandikishaji huo ni vyema pia kutii maagizo waliyopewa na kujitahidi kutunza vifaa,kufanya kazi kwa siri na  kujenga nidhamu itakayoweza kuwasaidia kufanya kazi pasina misuguano baina yao na kulitumikia taifa kwa uweledi katika kazi hio.

Alisema haitapendeza kumuona Karani wa Uandikishaji anatumia VRD nje ya malengo yanayokusudiwa kwani vifaa hivyo vinahitaji  kutumika kwa uangalifu mkubwa “naomba nitumie fursa hii kwa mara nyengine tena kuwakumbusha kuwa mnakwenda kufanya kazikatika jamii tofauti kwenu nikuhakikisha mnatoa huduma bora ilisisi tuliokutumeni tuweze kujifariji.

Bi. Mwanakombo aliwasihi kuwa kuwasimamia vyema watu  wenye mahitaji maalum kama vile wazee , watu wenye ulemavu au mama wajawazito ili nao waweze kupata  haki yao hio bila ya usumbufu.

Nae Afisa wa Uandikishaji Tume ya Uchaguzi Zanzibar  Wilaya Chakechake  Abdalla Juma  Abdalla aliwataka Waandikishaji hao kujenga mashirikiano mazuri na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ili kufanikisha zoezi hilo.

Tume ya uchaguzi Zanzibar inatarajia kuanza zoezi la kuandikisha Wapiga Kura Wapya tarehe 2 Disemba 2023  katika Wilaya  ya Micheweni ikiwa ni maandalizi ya uchaguzi Mkuu wa 2025.

Mawasiliano Yetu


Tume ya Uchaguzi Zanzibar

S.L.P 1001 - Zanzibar, Tanzania.

Simu: +255 242231489

Nukushi: +255 242233828

Mitandao ya Kijamii